Saturday 27 January 2018

Mzee Majuto ategua kitendawili Ugonjwa unaomsumbua


Mchekeshaji maarufu Bongo, Amri Athumani alimaarufu kama 'Mzee Majuto' amefunguka na kuweka wazi ugonjwa ambao unamsumbua kwa sasa kuwa ni tezi dume na kudai kuwa atafurahi sana endapo atafanyiwa upasuaji na kuondolewa maradhi hayo.
Mzee Majuto ambaye kwa sasa yupo jijini Dar es Salaam na tayari ameanza hatua za awali kuhakikisha kuwa anafanyiwa upasuaji kuondolewa tezi dume amesema kuwa kutokana na umri wake hashangazwi yeye kupata ugonjwa huo na kudai ni ugonjwa tu kama yalivyo magonjwa mengine. 
"Tayari nimeshafanyiwa vipimo kadhaa toka nilipofikishwa Muhimbili hapa saizi nasubiri siku ya Jumanne niende kuonana na daktari ambaye anashughulika zaidi na tezi dume ili aweze kusoma vipimo hivyo vizuri na kuona jinsi gani naweza kufanyiwa upasuaji. Huu ni ugonjwa wa kawaida na wapo watu wengi wameshaupata hata wengine nyinyi mnawajua sema mimi sitaki kuwataja tu hapa" alisema Mzee Majuto
Aidha Mzee Majuto ameshauri watu wengine ambao wana ugonjwa huo wa tezi dume kuhakikisha wanafanyiwa upasuaji mapema kabla ya njia za mkojo kuziba kwani ikifika hatua hiyo watapata shida sana. 
Mwaka jana Mzee Majuto alifanyiwa upasuaji akiwa mjini Tanga alipokuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa 'Hernia' lakini mwaka huu ameamua kuja Muhimbili jijini Dar es Salaam kufanyiwa upasuaji wa Tezi dume kutokana na ushauri wa madaktari baada ya kugundua kuwa ana tatizo la moyo.

0 comments:

Post a Comment