Siku
moja baada ya Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe (ACT Wazalendo)
kuanika mali zake na madeni kwenye mitandao ya kijamii na kuwataka
viongozi wengine wafanye hivyo, Katibu wa Bunge, Stephen Kigaigai,
amesema jambo hilo ni uamuzi binafsi wa mtu, hivyo ofisi yake haiwezi
kuingilia.
Pia
katibu huyo alisema kuwa bado hajauona muswada anaodai Zitto kuwa
tayari amewasilisha zaidi ya mara moja kutaka kuwapo kwa sheria
itakayowalazimisha wabunge na mawaziri kuweka wazi kwa umma taarifa juu
ya mali wanazomiliki pamoja na madeni yao na si taarifa hizo kuishia tu
kwa Kamishna wa Maadili.
Juzi,
kupitia kurasa za akaunti zake za mitandao ya kijamii ya facebook na
tweeter, Zitto aliweka hadharani tamko lake juu ya mali zote anazomiliki
pamoja na madeni, ikiwa ni muda mfupi baada ya kuliwakilisha na
kupokewa kwenye Ofisi ya Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
Jana ndiyo iliyokuwa siku ya mwisho kisheria kwa kila kiongozi kuwasilisha tamko lake kwenye sekretarieti hiyo.
Katika
tamko lake hilo, Zitto alitaja mali zake zinazoweza kuchukuliwa na
Watanzania walio wengi kuwa ni utajiri kutokana na hali halisi ya kipato
kwa wengi wao.
Mali
hizo ni pamoja na fedha taslimu Sh. milioni 55.2 zilizotokana na
mshahara; Sh. milioni 21.8 alizoingiza kupitia posho ya kujikimu; Sh.
milioni 102 zilizotokana na posho ya ubunge huku posho ya vikao ikiwa
sifuri kutokana na ukweli kuwa huwa hachukui.
Kadhalika,
Zitto alisema kwa ufupi, tamko lake la mwaka 2017 unaomalizika leo
halina tofauti sana na mwaka 2016 isipokuwa katika baadhi ya maeneo
ikiwamo kuongezeka kwa deni jipya kutoka Benki ya Azania kiasi cha Sh.
milioni 104 na deni la mtu binafsi kiasi cha dola za Marekani 2,300.
Pia
kupungua kwa madeni ya benki ya CRDB kutoka Sh. milioni 214 hadi
kufikia Sh. milioni 143 na NSSF kutoka Sh. milioni 191 hadi kufikia Sh.
milioni 142 baada ya kuyalipa kwa mwaka mzima uliopita; kuongezeka kwa
rasilimali ambazo ni hisa 60,000 za kampuni ya Vodacom na kupimwa kwa
ardhi eneo la Mangamba Manispaa ya Mtwara Mikindani lenye vitalu 42 vya
ukubwa tofauti.
Kuhusiana
na uamuzi wa Zitto wa kufichua maslahi yake kwenye kurasa za facebook
na tweeter, Kigaigai alisema mbunge huyo hawezi kuzuiwa kufanya hivyo
kwa sababu ni uamuzi wake binafsi.
“Hata
wewe (mwandishi) ukiamua kufanya hivyo ili mimi nijue, sioni kama kuna
tatizo… yeye kaamua (kwa utashi) binafsi na sidhani kama hilo lina
kizuizi,” alisema Kigaigai.
Kuhusiana
na madai ya Zitto kuwasilisha zaidi ya mara moja muswada wa sheria ya
kuwalazimisha wabunge na mawaziri kuweka hadharani tamko la mali zao na
madeni kwa nia ya kuimarisha maadili na kufanikisha zaidi dhana ya
utawala bora, Kigaigai alisema yeye hajaona muswada huo na wala
haufahamu.
“Huo
muswada mimi sijauona na wala siujui … katika ofisi hii sina muda mrefu
,” alisema Kigaigai ambaye aliteuliwa na Rais John Magufuli kuwa Katibu
wa Bunge Oktoba 7, mwaka huu.
0 comments:
Post a Comment