Friday 3 November 2017

Odinga awaasa wafuasi wake kususia bidhaa za kampuni tatu


Muungano wa upinzani nchini Kenya National Super Alliance (Nasa) umetoa wito kwa wafuasi wake kususia bidhaa na huduma kutoka kwa kampuni tatu ambazo unadai zimekuwa zikimpendelea Rais Uhuru Kenyatta.
Bw Kenyatta alitangazwa Jumatatu kuwa mshindi wa uchaguzi wa marudio uliofanyika 26 Oktoba, ambao kiongozi wa Nasa Raila Odinga alisusia akisema haungekuwa huru na wa haki.
Bw Odinga alitangaza kabla ya uchaguzi huo kwamba muungano huo utabadilika na kuwa Kundi la Pingamizi dhidi ya Serikali na baadhi ya hatua ambazo ulisema utachukua ni kususia bidhaa na huduma kutoka kwa kampuni ambazo alidai zinamfaa Bw Kenyatta.
Kampuni ambazo Nasa wamesema wafuasi wao wanafaa kususia ni:

•Kampuni ya mawasiliano ya Safaricom, ambayo ndiyo tajiri zaidi miongoni mwa kampuni za Kenya
•Kampuni ya maziwa ya Brookside, inayomilikiwa na familia ya Kenyatta
•Kampuni ya kutengeneza mafuta ya kupikia na sabuni ya Bidco
Safaricom leo ilitangaza Safaricom kukua kwa faida yake baada ya kutozwa ushuru kwa kipindi cha nusu mwaka kilichomalizika tarehe 30 Septemba kwa asilimia 9.5 hadi Sh26.2 bilioni.
Kampuni hizo kufikia sasa hazijazungumzia hatua hiyo ya upinzani ya kuwataka Wakenya kususia bidhaa na huduma zao.
Bw Odinga alisusia kushiriki uchaguzi huo wa mwezi uliopita akishinikiza mageuzi yafanywe kwanza katika Tume ya Taifa ya Uchaguzi.

0 comments:

Post a Comment