Saturday 20 January 2018

Benki Ya Dunia Yatoa Ufadhili Wa Shilingi Bil. 47 Kuhifadhi Rasilimali

 


Benki ya Dunia imetoa ufadhili wa shilingi Bilioni 47 kutekeleza mradi wa uhifadhi wa rasilimali za maji awamu ya pili katika bonde la mto Wami.

Akizindua mradi huo jana, Mjini Dodoma Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhandisi Isack Kamwelwe alisema kuwa Tanzania ina jumla ya mabonde tisa ya maji lakini mabonde hayo yameathiriwa kwa kiasi kikubwa na shughuli za kibinadamu na kiuchumi zinazosababisha kupungua kwa maji katika mabonde hayo.

"Fedha hizi zilizotolewa na Benki ya Dunia zitaenda kutoa elimu kuanzia ngazi ya juu mpaka mwananchi wa kawaida juu ya njia za kutumika kutunza rasimalimali za maji ndani ya hifadhi ya bonde la mto Wami," alisema Mhandisi Kamwelwe.

Aidha Mhandisi Kamwelwe amewataka wananchi na viongozi watakaopata elimu hiyo kutunza   rasilimali hiyo wao wenyewe kwa kutofanya shughuli za kibinadamu na za kiuchumi ndani ya hifadhi la bonde hilo.

Kwa upande wake, mwakilishi wa Benki ya Dunia Alex William amesema kuwa jukumu la utunzaji wa rasilimali za maji ni za kila mwananchi, kiongozi pamoja na taasisi za umma na binafsiHivyo amewata Watanzania kupitia mradi huo kutunza rasilimali hiyo ili kuongeza kiwango cha maji ndani ya bonde hilo ambayo yatatumika katika shughuli za nyumbani, viwandani, mashambani  katika shughuli za uvuvi pamoja na utalii.

Naye, Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji Mhandisi Nazifa Kemikimba amesema mradi huo utasaidia upatikanaji wa maji katika Jiji la Dar es Salaam na mikoa ya karibu ukiwemo mkoa wa Morogoro.

0 comments:

Post a Comment